Header Ads

Cup of coffee on saucer

SIFA BAINIFU ZA FIQHI KATIKA KIPINDI CHA BANI UMAYYAH



Image result for FIQHI ZA WANAZUONISifa Bainifu za Fiqhi katika Kipindi cha Banu Umayyah

Wanazuoni na wanafunzi katika dola ya Kiislamu katika kipindi hiki waligawanyika katika makundi mawili makubwa. Kundi moja la wanazuoni liliegemea katika upande wa kutoa maamuzi kwa kutumia Qur-aan au Sunnah, wakati kundi jingine lilifadhilisha kutumia ukubwa wa maamuzi ya kirai na Ijtihaad.
Kundi la kwanza lilikwepa kutoa hukumu za kisheria katika mambo ikiwa matini ya dhahiri kutoka kwenye Hadithi au Qur-aan inayohusiana na jambo hilo haipo. Msimamo huo uliegemezwa na maana ya wazi ya aya ya Qur-aan:

وَلاَ تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ

“Wala usiyafuate usiyo na ujuzi nayo” (17: 36).
Kanuni ambazo malengo yake yalitambuliwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) au Mtume Wake (Swalla Allahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) yalitumiwa katika Qiyaas[1] ilhali zile zilizoachwa bila kuelezwa hazikutumiwa. Kwa sababu ya msimamo huu, wanazuoni wa tapo hili la kifikra waliitwa Ahlul-Hadiyth (Watu wa Hadithi). Kituo kikuu cha wanazuoni wa Ahlul-Hadiyth kilikuwa ni Madiynah na Fiqhi ya shule ya Madiynah ilikuwa kwa sehemu kubwa, ni Fiqhi ya kimatendo na ikiegemea katika msingi wa matatizo ya hakika.
Kundi lengine la wanazuoni walihisi kuwa kanuni zote kadhaa zilizoteremshwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Mtume Wake (Swalla Allahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)  zilikuwa na mantiki, japo yawezekana mantiki hiyo imeainishwa na Allaah na Mtume wake au la. Katika hali ambazo sababu za kanuni hizo hazikuainishwa kwa maelezo, wanazuoni hawa walitumia juhudi zao za kiakili ili kufikia mantiki muafaka. Baadae walitumia kanuni hizo kwa hali nyenginezo zilizokuwa na mantiki kama hizo. Mwelekeo wao uliegemezwa na matendo ya baadhi ya Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum) wakubwa ambao walifikia hitimisho kwa kutoa sababu kwa baadhi ya kanuni za Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala). Kundi hili ambalo liliunga mkono utumiaji wa akili kwa kiasi kikubwa, walikuja kujulikana baadae kama Ahlur-Ra-ay (Watu wenye kutumia Akili). Kituo cha wanazuoni wa Ahlur-Ra-ay kilikuwa ni Kuufa, Iraq. Fiqhi ya Kuufa ilikua katika mipaka ya nadharia na dhana zaidi (isiyo na uhakika). Matatizo yalibuniwa na mbeya tofauti za hali zilizokuwepo kukisiwa, kisha utatuzi wa kubuni kufanyiwa kazi na kuandikwa. Katika majadiliano yao walikuwa mara nyingi wakitumia ibara, “Ingekuwaje lau ingekuwa hivi?” na hivyo walipatiwa pia jina la utani “Ingekuwaje”. Inatakiwa ifahamike kuwa mielekeo hii ilikuwa ni upanuzi wa mielekeo iliyotokea mwanzo miongoni mwa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum).

Post a Comment

No comments